Tunajifunza somo la kutetea Ukweli na Haki, na kuitokomeza batili kupitia Harakati ya Mapinduzi ya Imam Hussein (as), kiasi kwamba kila Muislamu na kila Mwanadamu aliye huru anapopinga batili, basi anakuwa anahuisha somo hilo la kihusseini.
Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Maadhimisho ya Arubaini ya Imam Hussein (a.s) yamefanyika katika Msikiti Mkubwa nchini Burundi ambapo Wafuasi na Wapenzi wa Imam Hussein (as), Mjukuu Kipenzi wa Mtume wao Muhammad (saww) wamekusanyika katika Msikiti huo kwa ajili ya Kusikiliza Khutba juu ya Mnasaba huo wa Maadhimisho ya Arubaini ya Imam Hussein (as) na Mashahidi wa Karbala.
Khutba hiyo iliyotolewa na: Sheikh Khamis Swadiq, ambaye alisisitiza katika Khutba yake juu ya umuhimu wa kuhuisha kumbukumbu ya Mjukuu wa Mtume wetu Muhammad (s.a.w.w) ambaye aliyeuawa Shahidi kwa ajili ya kuilinda na kuihuisha Dini Tukufu ya Uislamu.
Amesema kuwa Waislamu hupata mafundisho mengi kutoka katika harakati ya Imam Hussein (a.s), na miongoni mwa masomo makuu yanayoendelezwa kila mara na miaka yote kutoka katika Harakati ya Mapinduzi ya Karbala , ni kulinda, kutetea na kuhuisha Haki na Ukweli.
Sheikh Khamis Swadiq aliongeza kuwa Imam Hussein (a.s) kupitia Mapinduzi yake alimfundisha kila Mwanadamu somo la kutetea Ukweli na Haki, kiasi kwamba kila Muislamu na kila Mwanadamu aliye huru anapopinga batili, basi anakuwa anahuisha somo hilo la kihusseini.
Your Comment